Skip to main content
News and Events

WAZIRI MULAMULA: IMARISHENI BIASHARA KATI YA TANZANIA, DRC

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb.) ameutaka Ubalozi wa Tanzania nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) kuendelea na jitihada za kuwashawishi wafanyabiashara kutoka nchini humo kufanya zaidi biashara na Tanzania. Balozi Mulamula ametoa agizo hilo alipokutana kwa mazungumzo na Balozi wa Tanzania nchini Congo, Mhe. Juma Mshana katika Ofisi za Ubalozi nchini humo.

Balozi Mulamula, ametembelea Ubalozi huo mara baada ya kumalizika kwa Mkutano wa siku mbili wa Baraza la Mawaziri wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrka (SADC) uliofanyika Kinshasa nchini humo. Mkutano wa Mawaziri pamoja na mambo mengine huandaa agenda mbalimbali ambazo zitawasilishwa katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali kwa lengo la kuidhinishwa au kutolewa maamuzi.

Mkutano wa Kawaida wa 42 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) utafanyika tarehe 17 na 18 Agosti 2022 ambapo ujumbe wa Tanzania unatarajiwa kuongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan.

  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) akisaini katika kitabu cha Wageni katika Ubalozi wa Tanzania nchini DRC mara baada ya kuwasili katika ubalozi huo
  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Liberata Mulamula (Mb) akiwa katika kikao kazi na baadhi ya ujumbe wa Tanzania unaoshiriki katika Mkutano wa kawaida wa 42 wa Wakuu wa Nchi na Serikali unaotarajiwa kufanyika Agosti 17 na 18, 2022 Jijini Kinshasa, DRC