Skip to main content
News and Events

WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MAADHIMISHO UHURU WA TAIFA LA UTURUKI NA INDIA.

WAZIRI MULAMULA ASHIRIKI MAADHIMISHO UHURU WA TAIFA LA UTURUKI NA INDIA. 

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameshiriki hafla ya maadhimisho ya miaka 70 ya Uhuru wa India na miaka 98 ya Uhuru wa Taifa la Uturuki. Hafla hizo zilizoandaliwa na Ofisi za Ubalozi wa Mataifa hayo hapa nchini zimefanyika kwa nyakati tofauti jijini Dar es Salaam.   

Waziri Mulamula kwa nyakati tofauti akizungumza katika maadhimisho hayo amesifu mahusiano mazuri yaliyopo kati ya Mataifa hayo na Tanzania na ushirikiano katika maeneo mbalimbali ikiwemo sekta ya elimu, Afya, Kilimo, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, utalii, biashara na uwekezaji. Vilevile alielezea dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi mahiri wa Mhe. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jumhuri ya Muungano wa Tanzania wa kuendelea kuimarisha mahusiano mazuri yaliyopo na Mataifa hayo (India na Uturuki). 

“Tunashukuru Serikali ya India kwa msaada wa mradi wa usambazaji wa maji safi na salama katika miji 17 ya Tanzania ikiwemo katika maeneo ya jiji la Dar es Salaam na Chalinze. Vilevile kwa mradi wa upanuzi, ukarabati na uboreshaji wa huduma ya maji Zanzibar. Tanzania inaichukulia India kama moja ya washirika muhimu wa kimkakati kati ya Nchi za Asia” Alisema Waziri Mulamula

Kwa miaka  mingi Vyuo Vikuu vingi  vya nchini Uturuki vimetia saini Mikataba ya Makubaliano na Vyuo Vikuu vya nchini Tanzania ya kushirikiana katika kubadilishana programu, mafunzo na utafiti. Aidha, zaidi ya wanafunzi 400 wa Kitanzania wanaendelea na masomo yao nchini Uturuki katika fani mbalimbali ikiwemo udaktari, uhandisi na Sayansi. Ushirikiano huu umechangia kwa kiasi kikubwa kuendeleza mahusiano ya watu wa Mataifa haya mawili.  
 
Mwisho Waziri Mulamula alieleza kuwa Serikali ya Tanzania inaendelea na jitihada za kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini kwa kufanya marekebisho mbalimbali ya kisera na kisheria. Ametoa wito kwa Wafanyabiashara na Wawekezaji kutoka India na Uturuki na Mataifa mengine duniani kuja kuwekeza hapa nchini.

  • Balozi wa Comoron na Kiongozi wa Mabalozi hapa nchini Mhe. Ahamada El Badaoui Mohamed Fakih akihutubia kwenye maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam.
  • Hafla ya maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam ikiendelea.
  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) na Balozi wa Uturuki hapa nchini Mhe. Dr. Mehmet Gulluoglu wakiwa na mshindi wa tiketi ya ndege ya Turkish Airlines katika bahati nasibu iliyochezeshwa kwenye maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam.
  • Balozi wa Uturuki hapa nchini Mhe. Dr. Mehmet Gulluoglu akihutubia kwenye maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam.
  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (Mb) akihutubia kwenye maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam.
  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula (wa pili kushoto) akifuatilia onesho ya sanaa (hayapo pichani) yaliyokuwa yakiendelea kwenye maadhimisho ya 98 ya uhuru wa Taifa la Uturuki yaliyofanyika kwenye Ubalozi wa Taifa hilo jijini Dar es Salaam.