Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Dkt. Akinwumi Adesina amewasili jijini Dar Es Salaam
Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) anayemaliza muda wake, Dkt. Akinwumi Adesina amewasili jijini Dar Es Salaam kwa ziara ya kikazi ya siku 4 kuanzia tarehe 12 hadi 15 Juni 2025. Alipowasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere alipokewa na Waziri wa Kilimo,Mhe. Hussein Bashe na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki (EAC), Mhe. Denis Londo.
Wakati wa ziara hiyo, Dkt. Adesina anatarajiwa kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Aidha, Dkt. Adesina na Rais Samia watashiriki hafla ya ufunguzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Msalato na barabara ya mzunguko ya Dodoma jijini Dodoma tarehe 14 Juni 2025. Katika ziara hii, Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam kitamtunukia Shahada ya Heshima ya Falsafa Dkt. Adesina tarehe 13 Juni 2025.