Skip to main content
News and Events

BALOZI MULAMULA AKUTANA NA MWANA MFALME WA SAUDI ARABIA

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Liberata Mulamula, amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia Mwana Mfalme, Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud alipomtembelea katika Ofisi za Wizara hiyo jijini Riyadh- Saudi Arabia.

Katika mazungumzo yao Waziri Mulamula amemuhakikishia mwenyeji wake Mwana Mfalme, Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud kwamba Tanzania iko tayari kushirikiana na Saudi Arabia na kuendelea kuimarisha uhusiano mzuri uliopo kati ya nchi hizo.

Balozi Mulamula pia amemuhakikishia mwenyeji wake juu ya utayari wa Tanzania katika kufanya biashara na Saudi Arabia ikiwa ni pamoja na kuelezea fursa za uwekezaji zilizopo Tanzania kupitia sekta za mifugo, uvuvi, kilimo, utalii na usafiri wa anga.

Naye Mwana Mfalme, Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud alimuhakikishia Mhe Waziri juu ya nia na utayari wa Saudi Arabia kufanyabiashara na kuwekeza Tanzania kwa ajili ya kuzinufaisha nchi zote mbili.

Katika mazungumzo yao viongozi hao wamesisitiza umuhimu wa Tanzania na Saudi Arabia kuendelea kushirikiana na kuhakikisha biashara za uwekezaji vinashamiri baina ya nchi hizo.

Katika hatua nyingine Waziri Mulamula amekutana na viongozi wa Jumuiya ya wafanyabiashara na wenye viwanda wa Saudi Arabia jijini Riyadh na kuelezea fursa za biashara na uwekezaji zinazopatikana nchini na kuainisha maeneo ya kipaumbele kwa sasa.

Maeneo yaliyoainishwa kama kipaumbele katika kikao hicho ni pamoja na kilimo, mifugo, uvuvi, utalii na usafiri wa anga.

Waziri Muamula ametumia kikao hicho kuwaalika nchini wanachama wa jumuiya hiyo kwa ajili ya kushiriki Maonesho ya Kimaatafa ya Biashara ya Dar es Salaam maarufu Sabasaba yanayofanyika kila mwaka jijini Dar es Salaam mwezi Julai 

Viongozi wa jumuiya hiyo wameshukuru kupata nafasi ya kuonana na ugeni huo kutoka Tanzania ambao ulijumuisha Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki, Mwenyekiti wa Wafanyabiashara na wenye viwanda nchini (TCCIA) Mr. Joseph Koyi, kaimu Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) bibi Anna Lyimo na wawakilishi wa wafanyabiashara kutoka Tanzania Bara. 

 Waziri Mulamula na Ujumbe wake wako nchini Saudi Arabia kwa ziara ya kikazi kufuatia mwaliko wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia Mwana Mfalme, Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud, alioutoa mwezi Machi 2021 alipotembelea Tanzania.  

Katika ziara hiyo Balozi Mulamula ameambatana na Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki, Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro,  mwakilishi wa TAWA, Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) na wawakilishi wa Wafanyabiashara na Wenye Viwanda nchini.

Balozi Mulamula na ujumbe wake wanatarajia pia kukutana na viongozi wa Jumuiya ya Watanzania wanaoishi nchini Saudi Arabia, wafanyabiashara marafiki wa Tanzania wa jijini Riyadh na Jumuiya ya Wafanyabiashara katika miji ya Jeddah na Makkah atakaokutaana nao jijini Jeddah. Balozi Mulamula na ujumbe wake wanatarajia kurejea nyumbani tarehe 13 Machi 2022.

  • Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe Balozi Liberata Mulamula ukiwa nje ya Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje ya Saudi Arabia baada ya kumalizika kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia Mwana Mfalme, Mtukufu Faisal bin Farhan Al Saud ulipokwenda kuonana naye katika Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje ya Saudi Arabia jijini Riyadh
  • Ujumbe wa Tanzania ukikabidhi zawadi kwa Makamu mwenyekiti wa Shirikisho la wafanyabiashara na wenye viwanda nchini Saudi Arabia Bw. Tariq Al Haidary baada ya kikao na viongozi wa shirikisho hilo kilichofanyika katika Ofisi za Shirikisho hilo jijini Riyadh