Skip to main content
News and Events

BALOZI SOKOINE AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KWENYE MKUTANO WA NNE WA TUME YA USHIRIKIANO

BALOZI SOKOINE AONGOZA UJUMBE WA TANZANIA KWENYE MKUTANO WA NNE WA TUME YA USHIRIKIANO KATI YA TANZANIA NA KENYA ULIOFANYIKA JIJINI NAIROBI KWA NGAZI YA MAKATIBU WAKUU.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Joseph Sokoine  leo tarehe 23 Agosti 2021 ameongoza ujumbe wa Tanzania kwenye Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya kwa Ngazi ya Makatibu Wakuu uliofanyika jijini Nairobi

Pamoja na mambo mengine Mkutano wa Makatibu Wakuu umepitia na kuthibitisha agenda mbalimbali zilizowasilishwa kwao na Wataalam kabla ya agenda hizo kuwasilishwa na kupitishwa kwenye Mkutano wa Mawaziri unaotarajiwa kufanyika jijinii humo tarehe 24 Agosti 2021.

Kwenye hotuba yake ya ufunguzi wa Mkutano huo, Balozi Sokoine amewapongeza Wataalam kutoka Tanzania na Kenya kwa kukamilisha taarifa kwa wakati na kuwezesha mkutano wa makatibu wakuu kufanyika.

Alisema kuwa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano ni nyenzo muhimu katika kukuza ushirikiano kati ya nchi na nchi kwani hutoa fursa ya kuangalia maeneo ya ushirikiano kwa upana wake pamoja na kutoa nafasi ya kukubaliana maeneo ambayo ni ya kipaumbele na kuainisha mpango wa utekelezaji kwa ufanisi zaidi.

Pia aliongeza kuwa, Mkutano huo wa Nne utatoa nafasi kwa nchi hizi kutathmini namna makubaliano ya awali yalivyotekelezwa, kuainisha changamoto zilizojitokeza kwenye utekelezaji na kutoa suluhu ya namna ya kuzitatua ili kuimarisha ushirikiano uliopo kwa manufaa ya nchi hizi mbili na wananchi kwa ujumla. 

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Kenya, Balozi Macharia Kamau aliwakaribisha wajumbe kutoka Tanzania nchini Kenya na kuwataka wajumbe wote wa mkutano huo kupitia na kujadili taarifa zilizowasilishwa kwao kwa ufasaha ili kukamilisha jukumu hilo kwa ufanisi.

Mkutano wa Makatibu Wakuu ni mwendelezo wa maandalizi ya Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano unaotarajiwa kuhitimishwa na Mkutano wa Mawaziri hapo tarehe 24 Agosti 2021.



 

  • Meza Kuu wakifuatilia Mkutano wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya katika ngazi ya Makatibu Wakuu uliokuwa ukiendelea jijini Nairobi.
  • Ujumbe wa Tanzania ukifuatilia Mkutano wa wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya katika ngazi ya Makatibu Wakuu uliokuwa ukiendelea, jijini Nairobi.
  • Mkutano wa wa Nne wa Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na Kenya katika ngazi ya Makatibu Wakuu ukiendelea, jijini Nairobi.