Skip to main content
News and Events

BALOZI FATMA AFANYA MAZUNGUMZO NA UJUMBE WA WATAALAM WA UMOJA WA AFRIKA

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma Rajab leo terehe 11 Oktoba 2022 amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe wa Wataalam wa Umoja wa Afrika wa Kutathimini utekelezaji wa Agenda 2063, jijini Dodoma.

Ujumbe huo (Technical Working Group on the Evaluation of Agenda 2063) unaoongozwa na Bi. Josephine Etima upo ziarani nchini kuanzia tarehe 10 hadi 14 Oktoba 2022, ambapo utakutana na wadau mbalimbali wa Serikali katika ngazi ya wakurugenzi kwa lengo la kupata maoni yao kuhusu mpango wa utekelezaji wa Agenda 2063 katika kipindi cha muongo mmoja wa kwanza. 

Bi. Josephine na ujumbe wake ambao ulikutana na Balozi Fatma kwa lengo la kuelezea kuhusu ziara yao nchini, amebainisha kuwa maoni yatakayo tolewa na wataalam kuhusu mpango wa utekelezaji wa kipindi cha miaka 10 ya kwanza yatawasaidia kubaini musuala muhimu zaidi ya kuzingatia wakati wa kuandaa mpango wa pili wa miaka 10 ya utekelezaji wa Agenda 2063. 

Kwa upande wake Balozi Fatma akizungumza na ujumbe wa wataalam hao ameelezea hatua mbalimbali za maendeleo zilizofikiwa nchini ikiwa ni moja ya utekelezaji wa Agenda 2063. Ametaja baadhi ya maendeleo hayo kuwa ni pamoja na ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), mpango utoaji elimu bila malipo, uboreshwaji wa upatikanaji na usambazaji wa madawa na vifaa tiba na uboreshwaji wa huduma za afya vijijini. 

Mbali na hayo Balozi Fatma aliongeza kuwa jitihada zingine zinazofanywa na Serikali ya Tanzania katika kutekeleza Agenda 2063 ni pamoja na kuendesha programu mbalimbali zinazolenga kuwahamasisha Diaspora kushiriki katika shughuli za maendeleo nchini. Vilevile ameeleza kuwa Wizara na Serikali kwa ujumla inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kufanya biashara miongoni wa Waafrika wenyewe kupitia fursa zinazotokana na Eneo Huru la Biashara Barani Afrika (AfCFTA). 

Agenda 2063 ambayo imebeba kauli mbiu isemayo “Afrika Tuitakayo” ("The Africa We Want") inalenga pamoja na mambo mengine kuliunganisha Bara la Afrika katika masuala ya kukuza uchumi; kuhamasisha utawala bora na utawala wa sheria; kuhakikisha maendeleo kwa mtu mmoja mmoja; kuhakikisha amani na usalama unaimarika na kuiweka Afrika kwenye nafasi ya mchangiaji mkuu wa uchumi duniani

  • Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma Rajab (kulia) akiwa katika mazungumzo na na Bi. Josephine Etima kiongozi wa ujumbe wa Wataalam wa Umoja wa Afrika wa Kutathimini utekelezaji wa Agenda 2063, yaliyofanyika jijini Dodoma
  • Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma Rajab (mwenye kilemba) akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe wa Wataalam wa Umoja wa Afrika wa Kutathimini utekelezaji wa Agenda 2063 (kulia kwa Balozi Fatma) na Maafisa wa Wizara ya Mambo ya Nje (kushoto kwa Balozi Fatma)
  • Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Fatma Rajab (mwenye kilemba) akiwa katika mazungumzo na ujumbe wa Wataalam wa Umoja wa Afrika wa Kutathimini utekelezaji wa Agenda 2063