Skip to main content
News and Events

WAZIRI MULAMULA ASAINI KITABU CHA MAOMBOLEZO U.A.E

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), nchini kufuatia kifo cha Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan kilichotokea tarehe 13 Mei 2022.

Baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi wa UAE nchini, Jijini Dar es Salaam Balozi Mulamula ametoa salamu za pole kwa Serikali ya UAE na kuwasihi wananchi wake kuendelea kuwa watulivu wakati huu wa msiba wa kuondokewa na kiongozi wao.

“Kusaini kitabu cha maombolezo ni ishara ya ushirikiano, umoja na undugu wetu na ndugu zetu wa UAE. Kifo cha Rais wa UAE, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan kimewagusa pia Watanzania kwa kuwa Tanzania na UAE zina uhusiano mzuri,” alisema Balozi Mulamula.

Aliyekuwa Rais wa UAE, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan alifariki dunia tarehe 13 Mei, 2022 akiwa na umri wa miaka 73 baada ya kuugua kwa muda.

  • Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu nchini Mhe. Khalifa Abdulrahman Mohamed Al-Marzooqi akimueleza jambo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula baada ya kusaini kitabu cha maombolezo
  • Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu nchini Mhe. Khalifa Abdulrahman Mohamed Al-Marzooqi baada ya kusaini kitabu cha maombolezo katika Ubalozi huo kufuatia kifo cha Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Sheikh Khalifa bin Zayed Al-Nahyan kilichotokea tarehe 13 Mei 2022