Home » Highlights » Katibu Mkuu akanusha habari potoshi kuhusu Balozi zetu Nje |
|
Katibu Mkuu akanusha habari potoshi kuhusu Balozi zetu Nje
Posted: Wednesday February 15, 2012 10:18 AM BT
Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. John M. Haule (katikati), akikanusha na kurekebisha taarifa potoshi zilizoandikwa katika baadhi ya magazeti kuhusu Mabalozi na watumishi wake nje ya nchi. Pichani ni Bw. Lupakisyo Mwakitalima (Kulia), Mhasibu Mkuu Wizarani na Bw. Assah Mwambene (kushoto), Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
![]() Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. John M. Haule, leo alikutana na waandishi wa habari Wizarani, kukanusha na kusahihisha habari potoshi zilizoandikwa na baadhi ya magazeti. Machapisho ya baadhi ya magazeti hayo yaliandika kuwa Balozi za Tanzania nje ziko hoi, na kwamba Wizara haina fedha za kulipa mishahara, na hivyo kufanya watumishi kuishi kwa mikopo. Bw. Haule alieleza kuwa "taarifa hizo si sahihi na ni potoshi kwa umma." Alieleza kuwa ni kweli kuwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) ilikutana jana, na kwamba "si kweli kuwa Wizara haina fedha za kuwalipa mishahara Mabalozi au watumishi wake wa nje, bali fedha hizo zimetengwa na upelekwa Ubalozini mara zinapotolewa na Hazina." Aidha, alieleza kuwa Hazina imeanzisha utaratibu mpya ambapo Balozi zinatumiwa fedha zakukidhi mahitaji (mishahara na posho za kujikimu) mara moja kila baada ya miezi mitatu. Kwa mfano, kwa mwaka huu, Hazina imeshazituma fedha za miezi Januari, Februari na Machi. Sambamba na maelezo hayo, Bw. Haule alisema kuwa mfano alioutumia jana alipokuwa akihojiwa na Kamati ya PAC, ulikuwa ni kwa ajili ya kuonyesha kuwa fedha zilizolipwa na Hazina katika kipindi cha bajeti ya mwaka 2011/12 bado hazikidhi mahitaji ya Wizara. "Lakini kitendo cha baadhi ya magazeti kuripoti taarifa potoshi ni cha kusikitisha, na kwa kwamba Serikali kwa kupitia Wizara hii, utuma mishahara na psho kwa wakati kwa kadri zinapopokelewa kutoka Hazina. Tuna ushirikiano mzuri na Hazina, na tunafuata utaratibu mpya wa kutuma fedha uliopangwa na Hazina. Utaratibu huo ni wa kutuma fedha mara moja kila miezi mitatu," alieleza Bw. Haule. |